Majukumu ya Msingi

Majukumu ya msingi ya DIB kama yalivyoainishwa katika Sheria ya Mabenki na Taasisi za Fedha ya mwaka 2006 ni:

 

1.Tathmini na Ukusanyaji wa Michango

DIB inajukumu la kukusanya michango kutoka kwa benki na taasisi za fedha zinazopokea amana. Makadirio ya michango hufanyika mara moja kila mwaka kwa kuzidisha kiwango cha malipo cha asilimia 0.15 kwa wastani wa jumla ya amana za benki au taasisi za fedha zilizowekwa katika kipindi cha miezi kumi mbili kabla ya tarehe ya notisi ya malipo. Baada ya tathmini ya malipo kufanyika, malipo yanatakiwa kufanyika ndani ya siku 21 tangu tarehe ya notisi kutolewa kwa benki au taasisi za fedha.

 

2. Usimamizi wa Mfuko

DIB ina jukumu la kusimamia Mfuko wa Bima ya Amana (DIF). DIF hupata fedha zake kutokana na vyanzo vikuu viwili, yaani michango kutoka benki na taasisi za fedha zinazopokea amana na mapato ya riba kutokana na uwekezaji. Kwa kiasi kikubwa, rasilimali hizo huwekezwa katika dhamana zilizo chini ya udhamini wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, yaani Dhamana za Serikali na Hati fungani. Uwekezaji hutegemea muda wa kuiva kulingana na masharti yaliyowekwa katika Sera ya Uwekezaji ya DIB.

Wanachama wa mfuko

3. Ulipaji Fidia kwa Amana Zilizokingwa

DIB inalipa fidia wenye amana zilizokingwa endapo benki au taasisi ya fedha imeanguka. Kwa sasa (kuanzia tarehe 01 Februali,2023), amana zinakingwa hadi kufikia ukomo wa shilingi 7,500,000.00, sawa na kiasi cha dola za Marekani 3,250.00 kwa kila mwenye amana katika benki. Kiwango cha juu cha sasa cha shilingi 7,500,000 kinakinga asilimia 97.1 ya jumla ya idadi ya akaunti za amana. Ulipaji fidia kikamilifu kwa amana zilizokingwa unakuza imani ya umma katika mfumo wa kibenki na hivyo kuchangia katika utulivu wa sekta ya fedha nchini.

Ulipaji fidia kwa amana za benki  zilizofungwa unaendeshwa na DIB kwa kushirikiana na BOT kupitia ofisi kuu za benki zilizofungwa. Kwa upande wa iliyokuwa FBME Bank Limited, zoezi la malipo ya fidia linafanywa na DIB kupitia Ofisi za BOT nchini kote.

Kwa benki nyingine sita zilizo chini ya ufilisi  zoezi la ulipaji fidia ya Bima ya Amana linatekelezwa na  wakala aliyechaguliwa ambaye ni Tanzania Commercial Bank Plc (zamani TPB Bank Plc) kupitia mtandao wake mkubwa wa matawi nchi nzima chini. Hii ni kwa mujibu wa makubaliano kati ya DIB na Tanzania Commercial Bank Plc.

Fund Management Vorious Photo